Peter Kimath.
WAKATI Tanzania ikiwa na
wizara tatu kamili zinazoshughulikia masuala ya watoto, watoto wenye ulemavu
wamekuwa wakifichwa ndani na kukosa haki zao.
Wizara hizo ni pamoja na
iliyopo katika Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana,
Ajira na Walemavu na ile ya Wizara ya Afya, Maendeleo yaJamii, Jinsia, Wazee na
Watoto pamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi Teknolojia na Ufundi.
Watoto hao baadhi yao
wakiwa na ulemavu wa akili na viungo, wamekuwa wakifichwa katika wilaya ya
Mvomero, mkoani Morogoro.
Kufichwa kwa watoto hao
kunatokana na kule kunakoelezwa mila potofu, ukosefu wa elimu na ukandamizaji
wa haki za wenye ulemavu.
Mzee Luwi Faustine (81) mkazi wa kijiji cha
Makuyu Mvomero anasema kuwa familia nyingi tangu enzi za mababu zilikuwa
zikiua watoto wenye ulemavu pindi wanapozaliwa. Watoto hao walikuwa
wakiuawa kwa kile kinachodaiwa kuwa ni mkosi ndani ya familia.
Anasema kuwa tabia hiyo
ilijengeka katika familia, kutokana na imani kuwa mlemavu sio mtu anayestahili
kuishi duniani, amezaliwa na kasoro hivyo hatakiwi kuishi, kuonekana wala
kujulikana na familia nyingine.
“Hakuna mtu yeyote alikuwa
anatoa taarifa kuwa ana mtoto mlemavu ndani ya familia yake, kwa sababu
waliogopa kutengwa. Pia waliogopa kutoshirikishwa katika shughuli za maendeleo
ndani ya kijiji,”anabainisha Faustine.
Kulingana na Faustine,
baada ya kubaini ubaya wa kuua , walianza kutumia mbinu ya
kuwaficha watoto wenye ulemavu ndani, ili wasitambulike na mtu yeyote.
Anasema kuwa familia
nyingi zilifanikiwa zoezi la kuficha watoto ndani na kuwaua kwa kuwa akina mama
walikuwa wakijifungulia nyumbani, hivyo kuwa vigumu kutambua
familia zilizokuwa na watoto wenye ulemavu.
Faustine anaamini kuwa
inaweza kubadilika na kuachana na mila na desturi potofu kwa
kuelimishwa, hivyo kutambua kuwa mwenye ulemavu ana haki sawa na kuishi popote
huku akipata huduma zinazostahili.
Kwa upande mwingine anasema
kuwa endapo kutafanyika sensa maalum kwa ajili ya wenye ulemavu vijijini,
itaisaidia serikali kuwatambu na kutoa elimu ya kumlea mtoto mwenye
ulemavu pindi anapozaliwa, ili kuweza kupatiwa
msaada kwa urahisi, pia itasaidia kupunguza wimbi la watoto wanaofichwa ndani.
Kwa upande wake, Dkt.Hugo
Kapilima kutoka Hospitali ya SUA anasema tatizo la mtindio wa ubongo
(ulemavu wa akili) kwa watoto linasababishwa na vinasaba (Genetic), anavyokuwa
ametumia mama wakati wa ujauzito, hii hutokana na kina mama kutofuata taratibu
za lishe wanazopewa na wataalamu wa afya.
Dkt. Kapilima anasema kuwa
pombe na madawa ya kulevya vinakuwa na madhara makubwa, husababisha mtoto
kupata tatizo linalojulikana kitaalamu kama Fetal Alcoholic Syndrome (FAS).
Anasema matumizi ya madawa
ya kulevya, pombe kali, na dawa anazotumia mama wakati akiwa mjamzito,
zinachangia kujifungua mtoto mwenye itilafu katika ubongo.
Pia anasema upo uwezekano
mkubwa kwa mama kujifungua mtoto mwenye matatizo ya ubongo endapo atapata ajali
wakati wa ujauzito.
Anasema wanawake wamekuwa
na kawaida ya kutumia dawa za aina mbalimbali pindi wanapokuwa na ujauzito bila
kupata ushauri wa kitaalamu, jambo linalochangia mtoto kuzaliwa na tatizo la
akili.
Kijiji cha Makuyu kipo
katika Tarafa ya Mvomero, Wilaya ya Mvomero, kilomita 68 kutoka makao makuu ya
Wilaya,kuna watoto wenye ulemavu 48,watoto watano ni kutoka familia ya Lenat
Abdallah.
Mzee Lenat Abdallah (80)
mume wa Maria Lucas (56) anasema wanalazimika kuwasidia kila kitu watoto
wao watano wenye ulemavu wa akili na viungo.
Anasema watoto hao,
wanalishwa chakula, hujisadia haja ndogo na kubwa sehemu yoyote, miguu
imepinda,hawawezi kusimama na kutembea.
Kwa mujibu wa Abdallah,
mtoto wake wa kwanza Charles Lenat alizaliwa mwaka 1990 akiwa hana tatizo
lolote katika viungo vya mwili wake.
Anasema kuwa
alipofika umri wa miezi minne alianza kupatwa na homa za mara kwa mara na
walipompeleka hospitali ya Bwagala iliyopo Turiani vipimo vilionyesha kuwa
amepatwa na ugonjwa wa degedege.
Abdallah anasema kadri
mtoto huyo aliyokuwa anakua akawa hatoi sauti, kutembea wala kukaa
mwenyewe, jambo hilo liliwashtua sana na walipojaribu kumpeleka hospitali hali
haikubalika kabisa.
Anasema kuwa
alipofikisha miaka tisa miguu ilianza kuvimba na mpaka sasa mwanae huyo
mwenye umri wa miaka 26, hawezi kutembea,miguu imepinda, kuongea wala
kujihudumia kwa lolote akiwa peke yake.
Mwanae wa pili, Severine
Lenat alizaliwa mwaka 1993 akiwa mzima lakini alianza kupatwa na homa za
mara kwa mara akiwa na miezi miwili na walipomfikisha hospitali matokeo
yalionesha anasumbuliwa ugonjwa wa degedege.
Mtoto huyo alipata
matibabu ya awali katika hospitali ya Bwagala, lakini walishauriwa kumpeleka
hospitali ya mkoa wa Morogoro kwa matibabu zaidi. Hata hivyo, walishindwa
kufanya kumpatia matibabu kutokana na ukosefu wa fedha.
Anasema waliendelea
kuwatunza watoto wao wawili ndani bila hata majirani kujua kama watoto wao ni
walemavu wa akili na viungo, kwani walikuwa wanaona ni jambo la aibu kijijini,
haikuwahi kutokea katika familia yoyote.
Mtoto wa tatu wa
mzee Lenat Abdallah,Violet Lenat, alizaliwa mwaka 1997 akiwa mzima, lakini
alipofikia hatua ya kutembea, alianza kuumwa na walipomfikisha hospitali
waliambiwa anaumwa malaria.
“Tuliendelea kupata
matibabu katika hospital ya Bwagala iliyopo Turiani bila mabadiliko
yoyote. Kadri mtoto anavyokua tuliona haongei, alishindwa hata kutembea na
kuanza kutambaa tu chini hali aliyonayo hadi hivi sasa,” anasema.
Mtoto wake wanne,
Emmanuel Lenat alizaliwa mwaka 2000.- Emmanuel alizaliwa mzima ila
alipatwa na degedege akiwa na miezi mitatu. Tofauti na wenzake, Emmanuel
anaweza kutembea kidogo wakati wenzake waliotangulia kuzaliwa wanatambaa
tu chini.
Mtoto wa tano mwenye
ulemavu wa akili na viungo ni mjukuu wa mzee Lenat, Josephine Hermani. Mtoto
huyo alizaliwa salama, lakini alipofikisha miezi mitatu alianza kulia hovyo na
alipopelekwa hospitali kwa matibabu, hakuna msaada uliopatikana.
Anasema kuwa madkatari
hawakuwa na majibu sahihi ya ugonjwa wa mtoto, kwa kuwa walishaoona ni jambo la
kawaida kwa familia hiyo kuwa na watoto walemavu na kuwapa dawa za aina ya
asprini kutibu homa.
Josephine aliendelea kukua
katika hali ya kutokuongea, kutembea na kutojitambua kwa lolote. Mpaka sasa
anaishi maisha hayo kama watoto wenzake ndani ya familia hiyo.
“Nashukuru Mungu familia
haikunitenga nilipopata hawa watoto, walishirikiana nami kutafuta tiba ila
ilishindikana na mpaka unavyoona hali ilivyo sasa wote wanatambaa tu chini na
hawajitambui kabisa,” anasema Lenat.
Mama wa watoto hao, Maria
Lucas anasema kuwa kabla ya kukutana na mzee Lenat aliwahi kupata watoto
watatu, lakini hawakuwa na matatizo yoyote, mmoja wao ni mama mzazi wa Hermani.
Kwa mujibu wa Maria kupata
watoto wenye ulemavu ni mipango ya Mungu, hawezi kumkosoa Mungu, hivyo
wanaendelea kuishi na watoto wao katika hali zote bila kujali jamii inasemaje
kuhusu watoto wao.
Anasema kuwa
walikuwa wanapata shida sana kijijini hapo, kwani kila mtu alikuwa
anawanyooshea kidole kwa kitendo cha kuwa na watoto wenye ulemavu watano ndani,
jambo hilo lilichukuliwa kwa mtazamo tofauti.
Kutokana na hali hiyo,
baadhi ya familia badala ya kuwasaidia na kuwapa ushauri, ziliwatenga na
kutotoa ushikirikiano wowote kwa familia hiyo, na kuoina ni yenye
mkosi katika eneo hilo.
Aidha anasema aliyefanya
familia hiyo kutambulika na kuweza kupata misaada mbalimbali ni Asasi ya
Eric Memorial Foundation,inayojishughulisha na kulea watoto wenye ulemavu.
“Nashukuru viongozi wa
taasisi hiyo,inayoongozwa na Mama Josephine Bakita, kwani imekuwa ikinishauri
jinsi ya kuwalea watoto hawa”.
Dada wa watoto hao,
Sesilia Lenat anasema anapata shida kuwalea ndugu zake kutokana na wazazi wao
hivi sasa kuzeeka, kushindwa kuzalisha na hakuna msaada wowote wanapata
kutoka serikali.
“Ndugu mwandishi kwa siku
tunakula mlo mmoja tu. Hatuwezi kwenda shambani kulima na kuacha hawa watoto
wenyewe,”
“Tunaiomba serikali
itusaidie kwani hawa watoto wanamahitaji kama watoto wengine wasio na ulemavu,”
anasema Sesilia.
Anasema ipo haja kwa
serikali kuwa na mipango ya kusadia kundi la wenye ulemavu wa
viungo na akili waliopo vijijini ambao hawatambuliki, kuliko kuishia mijini na
kuwasaidia wenye ulemavu ambao wanajiweza wenyewe hata kwa kutoa sauti.
Mwenyekiti wa Kijiji cha
Makuyu, Kanurt Kikoti anakiri kuwa familia hiyo inaishi mazingira magumu sana,
na kwamba inapata misaada kutoka kwa watu binafsi na taasisi za dini ambazo
zinaguswa na hali ya familia hiyo.
Anasema kuwa serikali ya
kijiji imejipangakuhakikisha fedha zitakazotolewa na serikali,milioni 50 za
kila kijiji zilizotangazwa na Rais,Dkt.Magufuli zinawafikia wahusika,na familia
zenye mahitaji maalum kupewa kipao mbele.
Kikoti anasema kuwa kila
wakati wa mavuno huwa anaitisha mkutano wa kijiji na kuwahimiza wananchi
kuchangia chakula kwa ajili ya kusaidia familia mzee Lenat.
Anasema kuwa familia
hiyo kwa asimilia 90 inasaidiwa na watu binafsi wanaotoka nje ya kijiji hicho,
na baadhi ya majirani wanaowazunguka. Mzee Lenat na mkewe Maria, hivi sasa
wamezeeka, hivyo suala la kuwahudumia watoto wao linawapa shida sana.
Anaongeza kuwa familia
hiyo inahitaji msaada mkubwa, serikali na wizara husika inapaswa kuzitupia
macho familia zenye watoto wenye ulemavu pamoja na kutembelea mazingira
wanayoishi vijijini.
Kwa upande wake Mshauri wa
Asasi ya Eric Memorial Foundation, Josephine Bakita anasema kuwa jambo kubwa
wanalolifanya ni kutoa elimu ya kuwalea watoto wenye ulemavu wilayani Mvomero.
Anasema elimu hiyo hutoa
kwa kupita nyumba kwa nyumba, kuwakusanya katika kundi moja ndani ya kijiji na
kuwapa elimu mara kwa mara,kutambua kundi la wenye ulemavu na kuona thamani
yao.
Josephine anasema kuwa
kundi la watu wenye ulemavu wa akili na viungo limetengwa, walioko vijijini
hawapati huduma za shule, afya, kama wenye ulemavu walioko mijini,
“Familia ya Mzee Lenat
yenye watoto watano wenye ulemavu wa akili na viungo, tumeitambulisha kwa wadau
mbalimbali ambao wanatoa misaada kwao.” anasema Josephine.
Anasema kuwa serikali
inapaswa kuweka mikakati ya kuwasaidia walemavu wa vijijini, kwa kuwatumia
maafisa ustawi wa jamii kutembelea familia zenye watoto wenye ulemavu na kutoa
elimu ya malezi.
Anasema kwa jinsi hali
ilivyo, watoto wengi wenye ulemavu hawaogeshwi kutokana na wanafamilia
kuwaogopa, hivyo kukumbwa na magonjwa ya ngozi.
Wakati watoto hao wenye
ulemavu wakiachwa bila kuthaminiwa, ipo haja kwa wizara husika za Sera, Bunge,
Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu na ile ya Wizara ya Afya, Maendeleo yaJamii,
Jinsia, Wazee na Watoto pamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi Teknolojia na
Ufundi, kusimama kidete kutetea maisha ya watoto wenye ulemavu.
Hakutakuwa na maana,
watoto wenye ulemavu kuendelea kutaabika na kusahaulika, wakati serikali ya
awamu ya tano imeunda wizara tatu, mahsusi kwa ajili yao..
Familia ya Lenat Abdallah iliyopo kijiji cha Makuyu wilayani Mvomero,familia hii ina watoto watano,wenye ulemavu wa viungo na akili. |
No comments:
Post a Comment