Friday, July 19, 2013

WANASHERIA NCHINI WATAKIWA KUTUMIA ELIMU YAO MAENEO YA VIJIJINI.




WANASHERIA nchini wametakiwa kutumia elimu waliyo nayo  katika kuelimisha jamii iishiyo vijijini kutokana na kuwa na uelewa mdogo  katika kujua mambo mbalimbali ya kisheria  ikiwemo kujua sheria na haki zao. 

Mwito huo umetolewa na  Mwanasheria Mshauri, Mtafiti na Mtetezi wa Haki za Binadamu Mkoani Morogoro,Amani Mwaipaja ,ambapo alisema kuwa utambuzi wa sheria umekuwa changamoto kubwa sana katika maeneo ya vijijini

Mwaipaja alisema kuwa  wasomi wengi wamekuwa wakikimbilia mjini wakiamini kuwa ndiko kwenye maslahi zaidi lakini wanasahau kuwa kujitolea kusaidia jamii ni sehemu ya kujiajiri kwa kuwa jamii kubwa hasa ya maeneoo ya vijijini inakabiliwa na changamoto nyingi za kisheria.

Alisema kuwa changamoto hizo ni pamoja na migogoro ya ardhi, masuala ya ndoa na talaka, 
migogoro ya mirathi pamoja na ugumu wa upatikanaji wa huduma za kisheria ambapo wananchi wengi hulazimika kutembea umbali mrefu kuitafuta huduma hiyo.



“Nawaomba wasomi wa sheria mtumie muda wenu katika kubuni njia rahisi ya kusambaza elimu ya sheria katika maeneo ya vijijini kwa kutumia vyombo vya habari  kwani vina nafasi kubwa sana katika jamii”alisema Mwaipaja.



Aliwataka wasomi kuandika vitabu vya sheria kwa lugha ya kiswahili pamoja na kutayarisha vipeperushi  na vijarida vitakavyomsaidia mwananchi wa kawaida kuelewa haki zake na kuzifuatilia



Katika kuonyesha mfano kwa wasomi, Mwanasheria Mwaipaja ametoa kitabu cha Zijue Sheria na Haki Zako, ambacho kinaelezea kuhusu shera na taratibu mbalimbali anazopaswa kuzifuata mwananchi ili aweze kupata haki zake. kitabu cha Zijue Sheria na Haki Zako tayari kimeanza kusambazwa katika wilaya zote za Mkoa wa Morogoro.



Mwisho

No comments:

Post a Comment